Bad Advertisement?

News / Reviews:
  • World News
  • Movie Reviews
  • Book Search

    Are you a Christian?

    Online Store:
  • Visit Our eBay Store



  • SWAHILI BIBLIA - LUKE 1

    JANA SURA - IJAYO SURA - AMARA


    1:1 Mheshimiwa Theofilo: Watu wengi wamejitahidi kuandika juu ya mambo yale yaliyotendeka kati yetu.

    1:2 Waliandika kama tulivyoelezwa na wale walioyaona kwa macho yao tangu mwanzo, na waliotangaza ujumbe huo.

    1:3 Inafaa nami pia, Mheshimiwa, baada ya kuchunguza kwa makini mambo yote tangu mwanzo, nikuandikie kwa mpango,

    1:4 ili nawe uweze kujionea mwenyewe ukweli wa mambo yale uliyofundishwa.

    1:5 Wakati Herode alipokuwa mfalme wa Yudea, kulikuwa na kuhani mmoja jina lake Zakaria, wa kikundi cha Abia. Mke wake alikuwa anaitwa Elisabeti, naye alikuwa wa ukoo wa kuhani Aroni.

    1:6 Wote wawili walikuwa wanyofu mbele ya Mungu, wakiishi kwa kufuata amri na maagizo yote ya Bwana bila lawama.

    1:7 Lakini hawakuwa wamejaliwa watoto kwa vile Elisabeti alikuwa tasa, nao wote wawili walikuwa wazee sana.

    1:8 Siku moja, ilipokuwa zamu yake ya kutoa huduma ya ukuhani mbele ya Mungu,

    1:9 Zakariya alichaguliwa kwa kura, kama ilivyokuwa desturi, kuingia hekaluni ili afukize ubani.

    1:10 Watu, umati mkubwa, walikuwa wamekusanyika nje wanasali wakati huo wa kufukiza ubani.

    1:11 Malaika wa Bwana akamtokea humo ndani, akasimama upande wa kulia wa madhabahu ya kufukizia ubani.

    1:12 Zakariya alipomwona alifadhaika, hofu ikamwingia.

    1:13 Lakini malaika akamwambia, "Zakariya, usiogope, kwa maana sala yako imesikilizwa, na Elisabeti mkeo atakuzalia mtoto wa kiume, nawe utampa jina Yohane.

    1:14 Utakuwa na furaha kubwa na watu wengi watashangilia kwa sababu ya kuzaliwa kwake.

    1:15 Atakuwa mkuu mbele ya Bwana. Hatakunywa divai wala kileo, atajazwa Roho Mtakatifu tangu tumboni mwa mama yake.

    1:16 Atawaelekeza wengi wa watu wa Israeli kwa Bwana Mungu wao.

    1:17 Atamtangulia Bwana akiongozwa na nguvu na roho kama Eliya. Atawapatanisha kina baba na watoto wao; atawafanya wasiotii wawe na fikira za uadilifu, na hivyo amtayarishie Bwana watu wake."

    1:18 Zakariya akamwambia huyo malaika, "Ni kitu gani kitakachonihakikishia jambo hilo? Mimi ni mzee, hali kadhalika na mke wangu."

    1:19 Malaika akamjibu, "Mimi ni Gabrieli, nisimamaye mbele ya Mungu, na nimetumwa niseme nawe, nikuletee hii habari njema.

    1:20 Sikiliza, utakuwa bubu kwa sababu huyasadiki haya maneno yatakayotimia kwa wakati wake. Hutaweza kusema mpaka hayo niliyokuambia yatakapotimia."

    1:21 Wakati huo, wale watu walikuwa wanamngoja Zakariya huku wakishangaa juu ya kukawia kwake Hekaluni.

    1:22 Alipotoka nje, hakuweza kusema nao. Ikawa dhahiri kwao kwamba alikuwa ameona maono Hekaluni. Lakini akawa anawapa ishara kwa mikono, akabaki bubu.

    1:23 Zamu yake ya kuhudumu ilipokwisha, alirudi nyumbani.

    1:24 Baadaye Elisabeti mkewe akapata mimba. Akajificha nyumbani kwa muda wa miezi mitano, akisema:

    1:25 "Hivi ndivyo alivyonitendea Bwana; ameniangalia na kuniondolea aibu niliyokuwa nayo mbele ya watu."

    1:26 Mnamo mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu aende kwenye mji uitwao Nazareti huko Galilaya,

    1:27 kwa msichana mmoja aitwaye Maria, mchumba wa mtu mmoja jina lake Yosefu, wa ukoo wa Daudi.

    1:28 Malaika akamwendea, akamwambia, "Salamu Maria! Umejaliwa neema nyingi! Bwana yu pamoja nawe."

    1:29 Maria aliposikia maneno hayo alifadhaika sana, akawaza: maneno haya yanamaanisha nini?

    1:30 Malaika akamwambia, "Usiogope Maria, kwa maana Mungu amekujalia neema.

    1:31 Utachukua mimba, utamzaa mtoto wa kiume na utampa jina Yesu.

    1:32 Yeye atakuwa mkuu na ataitwa Mwana wa Mungu Mkuu. Bwana Mungu atampa kiti cha mfalme Daudi, babu yake.

    1:33 Kwa hivyo atautawala ukoo wa Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho."

    1:34 Maria akamjibu, "Yatawezekanaje hayo, hali mimi ni bikira?"

    1:35 Malaika akamjibu, "Roho Mtakatifu atakushukia, na uwezo wake Mungu Mkuu utakujia kama kivuli; kwa sababu hiyo, mtoto atakayezaliwa ataitwa Mtakatifu, Mwana wa Mungu.

    1:36 Ujue pia kwamba hata Elisabeti, jamaa yako, naye amepata mimba ingawa ni mzee, na sasa ni mwezi wa sita kwake yeye ambaye watu walimfahamu kuwa tasa.

    1:37 Kwa maana hakuna jambo lisilowezekana kwa Mungu."

    1:38 Maria akasema, "Mimi ni mtumishi wa Bwana, nitendewe kama ulivyosema." Kisha yule malaika akaenda zake.

    1:39 Siku kadhaa baadaye, Maria alifunga safari akaenda kwa haraka hadi mji mmoja ulioko katika milima ya Yuda.

    1:40 Huko, aliingia katika nyumba ya Zakariya, akamsalimu Elisabeti.

    1:41 Mara tu Elisabeti aliposikia sauti ya Maria, mtoto mchanga tumboni mwake Elisabeti akaruka. Naye Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifiu,

    1:42 akasema kwa sauti kubwa, "Umebarikiwa kuliko wanawake wote, naye utakayemzaa amebarikiwa.

    1:43 Mimi ni nani hata mama wa Bwana wangu afike kwangu?

    1:44 Nakwambia, mara tu niliposikia sauti yako, mtoto mchanga tumboni mwangu aliruka kwa furaha.

    1:45 Heri yako wewe uliyesadiki kwamba yatatimia yale Bwana aliyokwambia."

    1:46 Naye Maria akasema,

    1:47 "Moyo wangu wamtukuza Bwana, roho yangu inafurahi kwa sababu ya Mungu Mwokozi wangu.

    1:48 Kwa kuwa amemwangalia kwa huruma mtumishi wake mnyenyekevu. Hivyo tangu sasa watu wote wataniita mwenye heri.

    1:49 Kwa kuwa Mwenyezi Mungu amenitendea makuu, jina lake ni takatifu.

    1:50 Huruma yake kwa watu wanaomcha hudumu kizazi hata kizazi.

    1:51 Amefanya mambo makuu kwa mkono wake: amewatawanya wenye kiburi katika mawazo ya mioyo yao;

    1:52 amewashusha wenye nguvu kutoka vitu vyao vya enzi, akawakweza wanyenyekevu.

    1:53 Wenye njaa amewashibisha mema, matajiri amewaacha waende mikono mitupu.

    1:54 Amemsaidia Israeli mtumishi wake, akikumbuka huruma yake.

    1:55 Kama alivyowaahidia wazee wetu Abrahamu na wazawa wake hata milele."

    1:56 Maria alikaa na Elisabeti kwa muda upatao miezi mitatu, halafu akarudi nyumbani kwake.

    1:57 Wakati wa kujifungua kwake Elisabeti ulifika, akajifungua mtoto wa kiume.

    1:58 Jirani na watu wa jamaa yake walipopata habari kwamba Bwana amemwonea huruma kubwa, walifurahi pamoja naye.

    1:59 Halafu siku ya nane walifika kumtahiri mtoto, wakataka kumpa jina la baba yake, Zakariya.

    1:60 Lakini mama yake akasema, "La, sivyo, bali ataitwa Yohane."

    1:61 Wakamwambia, "Mbona hakuna yeyote katika ukoo wake mwenye jina hilo?"

    1:62 Basi, wakamwashiria baba yake wapate kujua alitaka mtoto wake apewe jina gani.

    1:63 Naye akaomba kibao cha kuandikia, akaandika hivi: "Yohane ndilo jina lake." Wote wakastaajabu.

    1:64 Papo hapo midomo na ulimi wake Zakariya vikafunguliwa, akawa anaongea akimsifu Mungu.

    1:65 Hofu ikawaingia jirani wote, na habari hizo zikaenea kila mahali katika milima ya Yudea.

    1:66 Wote waliosikia mambo hayo waliyatafakari mioyoni mwao wakisema: "Mtoto huyu atakuwa mtu wa namna gani?" Maana, hakika nguvu ya Bwana ilikuwa pamoja naye.

    1:67 Zakariya, baba yake mtoto, akajazwa Roho Mtakatifu, akatamka ujumbe wa Mungu:

    1:68 "Asifiwe Bwana Mungu wa Israeli, kwani amekuja kuwasaidia na kuwakomboa watu wake.

    1:69 Ametupatia Mwokozi shujaa, mzawa wa Daudi mtumishi wake.

    1:70 Aliahidi hapo kale kwa njia ya manabii wake watakatifu,

    1:71 kwamba atatuokoa mikononi mwa adui zetu na kutoka mikononi mwa wote wanaotuchukia.

    1:72 Alisema atawahurumia wazee wetu, na kukumbuka agano lake takatifu.

    1:73 Kiapo alichomwapia Abrahamu baba yetu, ni kwamba atatujalia sisi

    1:74 tukombolewe kutoka adui zetu, tupate kumtumikia bila hofu,

    1:75 kwa unyofu na uadilifu mbele yake, siku zote za maisha yetu.

    1:76 Nawe mwanangu, utaitwa, nabii wa Mungu Mkuu, utamtangulia Bwana kumtayarishia njia yake;

    1:77 kuwatangazia watu kwamba wataokolewa kwa kuondolewa dhambi zao.

    1:78 Mungu wetu ni mpole na mwenye huruma. Atasababisha pambazuko angavu la ukombozi litujie kutoka juu,

    1:79 na kuwaangazia wote wanaokaa katika giza kuu la kifo, aongoze hatua zetu katika njia ya amani."

    1:80 Mtoto akakua, akapata nguvu rohoni. Alikaa jangwani mpaka alipojionyesha rasmi kwa watu wa Israeli.

    IJAYO SURA - BIBLIA MWELEZO & UTAFUTAJI

    God Rules.NET
    Search 100+ volumes of books at one time. Swahili Biblia Search Engine. Hausa Biblia Search Engine. Afrikaan Bible Search Engine